Ajira kwa Watoto nchini Tanzania, ni suala mtambuka ambalo linaendelea kupigwa vita zaidi. Hali sasa inaonyesha bado watoto wa kike ndio hasa waathirika wakubwa kulinganisha na watoto wa jinsia ya kiume.

Nchini Tanzania, ajira nyingi za watoto ziko katika mifumo mbalimbali . Mifumo ya wafanyakazi wa ndani, wafanyakazi wa mashambani, ombaomba na wanaofanyishwa biashara za ngono. Ajira hizi zinaathiri sana watoto kwani wanashindwa kukua kiakili lakini pa wanashindwa kuhudhuria masomo.

SOMA ZAIDI:

Hali ya Ajira kwa Watoto kulingana na ripoti mbalimbali

Kwa mujibu wa chapisho la kituo cha kutetea haki za binadam nchini Tanzania (Legal and Human Right Center) kuna jumla ya watoto 152 milioni wanafanyishwa kazi duniani kote na hawapati nafasi ya kuhudhuria shule, wengi wao wakitumikishwa katika sekta ya kilimo

Ripoti yam waka 2014 ya ILO kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaonyesha kuwa zaidi ya 84.2% ya watoto wa kike kwenye idadi ya jumla ya watoto Milioni 14.7 ya watoto wote nchini wanafanya kazi za ndani (Domestic servants) kulinganisha na 15.8% ya watoto wa kiume

Moja ya kazi za True Vision Production kuhusu Child labour

Sheria mbalimbali zinazomlinda mtoto katika kazi

Sheria ya Mtoto, Namba 21 ya mwaka 2009 inatoa maana ya mtoto kuwa ni mtu yeyote mwenye umri wa miaka chini ya 18. Pia inatoa ufafanuzi kuwa ukatili kwa watoto unajumuisha ajira kwa watoto ikiwemo ajira zinazowanyonya watoto.

Kifungu cha 4 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano ya Kazi ya mwaka, 2004. Kinamuelezea mtoto kama mtu mwenye umri chini ya miaka 14 isipokuwa kwa ajira zilizo katika sekta hatarishi, mtoto maana yake ni mtu mwenye umri wa chini ya miaka 18.

Kifungu cha 12 cha Sheria ya Mtoto kinaeleza kuwa mtoto hatahusishwa katika kazi yoyote ambayo inaweza kumsababishia madhara kiafya, kielimu, kiakili, kimwili na katika ukuaji wake. Ni kosa la jinai kumuajiri mtoto katika kazi zisizofaa na zenye madhara. Kama ilivoelezwa na Sheria ya ajira na Mahusiano Kazini katika kifungu cha 5.

Hata hivyo, sheria inaruhusu ajira kwa watoto wa miaka 14 katika kazi nyepesi ambazo sio hatarishi kwa afya ya watoto na maendeleo. Na haihatarishi mahudhurio ya watoto shuleni, mafunzoni au programu za kujifunza. Kwa ujumla ustawi wa watoto hautakiwi kuhatarishwa hata kidogo.

Mwaka 2017, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipiga hatua kubwa ya kuondoa ajira kwa watoto. Serikali ilitoa machapisho ya kisheria kuelezea kwa undani kazi hatarishi kwa watoto katika sekta mbalimbali. Kwa mara ya kwanza ikazuia shughuli hatarishi kwa watoto kwenye sekta ya uvuvi.

Duniani kote siku ya kupinga Ajira kwa Watoto inaadhimishwa tarehe 12 mwezi Juni kila mwaka. Siku hii ilianzishwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2002 kwa dhumuni la kutoa elimu na kufanya utetezi kuzuia ajira kwa watoto.

True Vision Production imekuwa ikijihusisha kwenye program na miradi mbalimbali ya kijamii. Huu ni mradi mmoja wapo wa kuhamasisha kupinga ajira kwa watoto.