Kampuni ya True Vision Production (TVP) imetoa msaada wa vitu mbalimbali kwa kituo cha watoto wenye uhitaji cha Moyo Mmoja kilichopo wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.

TVP ni kampuni ya Kitanzania inayojihusisha na utengenezaji wa vipindi, makala na matangazo kwa njia ya video na redio na hufanya kazi za serikali, mashirika na taasisi mbalimbali za binafsi, Kitaifa na Kimataifa.

Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo iliyojumuisha nguo za rika mbalimbali, vyakula vikiwemo unga, mchele, sukari, mafuta, sabuni ikiwa ni pamoja na michezo ya watoto, Mkurugenzi wa TVP, David Sevuri amesema kampuni hiyo imeamua kurudisha kwa jamii (CSR) kama sehemu ya utamaduni wake.

“Tumeamua kuuanza mwaka mpya kwa kutembelea kituo cha Moyo Mmoja, kutoa tulichojaaliwa na Mwenyezi Mungu, lakini kikubwa zaidi kukaa, kufurahi na kula nao kama sehemu ya familia,” amesema Sevuri.

TVP Moyo Mmoja

Wafanyakazi wa kampuni ya True Vision Production (TVP) wakiwa katika picha ya pamoja na watoto na walezi wa kituo cha kulelea watoto cha Moyo Mmoja kilichopo wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani walipokwenda kutoa misaada mbalimbali.

Sehemu kubwa ya msaada huo imetolewa na ofisi, huku wafanyakazi pia wakitoa misaada binafsi kwa jinsi walivyoguswa.

Sevuri amesema TVP ina utamaduni wa kurudisha kwa jamii sehemu ya kipato chake inachokipata kutokana na kazi mbalimbali inazozifanya, hivyo amewashukuru wateja(clients) kwa kuendelea kuiamini TVP na kufanya kazi pamoja.

“Tunawashukuru wateja wetu na tumeweza kulifanya hili kwa sababu ya kuwa pamoja nao na tunawaahidi kuwapa huduma nzuri kwa kutumia teknolojia ya kisasa zaidi.

Naye Godwin Kalambile, meneja msaidizi wa kituo hicho ameishukuru TVP kwa msaada huo, lakini kikubwa amefarijika kwa wafanyakazi hao kutenga muda wa kukaa, kufurahi na kula pamoja na watoto hao.

Wafanyakazi wa kampuni ya True Vision Production (TVP) wakimlisha mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo cha Moyo Mmoja kilichopo wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani wakati wa chakula kilichoandaliwa kwa ajlli ya wa watoto hao

Amesema kituo hicho kilianza mwaka 1998 baada kumuokota mtoto mchanga aliyetupwa na mama yake ili achukuliwe na maji katika fukwe za Coco Beach, jijini Dar es Salaam alipokuwa akifanyazi kazi kwa wakati huo.

“Ilikuwa ni usiku, tukiwa tumekaa tulisikia mbwa anabweka sana kuashiria kitu,”

“Mlinzi alinifuata na kuniomba tukaangalie kuna nini,”
“Chakusikitisha, tulikuta mtoto mchanga amefukiwa pembeni kidogo ya bahari ili usiku maji yakirudi yamsombe akafie baharini,”

“ Tulimchukua mtoto yule na baadae wasamaria wema walimchukua na kumlea na sasa hivi ni kijana mkubwa. Hapa ndipo Moyo Mmoja ilipoanzia,’ amesema.

Moja wa walezi wa kituo cha kulelea watoto cha Moyo Mmoja kilichopo Bagamoyo, mkoani Pwani, bibi Pili Athumani ( mama Mlekwa) akiwa na mmoja wa watoto wa kituoni haps wakati walipotembelewa na kampuni ya True Vision Production (TVP) kwa ajili ya kutoa misaada mbalimbali.

Kituo cha Moyo Mmoja kinalea watoto wadogo na wakubwa ambao wengi wao hupokelewa kituoni hapo wakiwa watoto wachanga wa siku mbili au tatu ambao sasa hivi wengi wao wanasoma sekondari na vyuo mbalimbali.

Pili Athumani, mmoja wa walezi wa kituo hicho ameishukuru TVP, huku akisema misaada hiyo imekuja kwa wakati.

“Kuna wakati tunakosa hata sukari, lakini Mungu amewaleta nasi tunawaombea,”

Watoto wa kituo cha kulelea watoto cha Moyo Mmoja kilichopo Bagamoyo, mkoani Pwani wakicheza muziki baada ya chakula cha mchana kilichoandaliwa na Kampını ya True Vision Production (TVP) ilipowatembelea kutoa misaada mbalimbali

Katika kituo hicho, watoto wote wanaishi kama família moja, huku walezi wakiwa wamegawana majukumu ya kuwalea watoto hao kulingana na umri wao.

Akiongea kwa niaba ya watoto wenzake, Mlekwa Moyo Mmoja( aliyelelewa kituoni hapo toka akiwa mchanga) na sasa anasoma kidato cha sita ameishukuru TVP, huku akiomba watu wengine wenye moyo wa kusaidia kujitokeza na kusaidia jamii.